Sehemu ya 2.2 Michango isiyo ya moja kwa moja ya serikali ya Marekani kuelekea Kenya

Biashara, uwekezaji, na wafanyakazi wenye ujuzi ni viungo muhimu katika juhudi za Kenya za kuwa taifa linalopiga hatua kwa kasi kufikia lengo la kuwa na uchumi wa viwanda na kipato cha kati ifikapo 2030. [17] Katika kila moja ya nyanja hizo, serikali ya Marekani ni mshirika muhimu katika kuunda mazingira ya kuwezesha Kenya kuwa na uchumi wa kisasa. Katika sehemu hii, tunachunguza jinsi sera bora za Marekani za biashara, uhamiaji, na uwekezaji zinavyosaidia Kenya kubadilisha uchumi wake kulingana na Ruwaza ya 2030.

Kilichogunduliwa 4: Sheria ya Maendeleo na Fursa kwa Afrika (The African Growth and Opportunity Act) iliiwezesha Kenya kuongeza idadi ya bidhaa nje zilizouzwa nchini Marekani kwa asilimia 285 kati ya 2000 na 2018.

Tangu miaka ya 1980, Kenya imechukua hatua nyingi ili kukuza uchumi ulio huru kwa kubadilisha sera mbalimbali za kibiashara na kiuchumi (Zepeda et. al., 2009). Hivi majuzi, Rais Uhuru Kenyatta alisema kwamba Kenya inahitaji kuimarisha uzalishaji au utengenezaji wa bidhaa viwandani na biashara nje kama mojawapo ya vitu vinne muhimu kwenye mpango wa Ruwaza ya 2030 ya Kenya. Nchi ya Marekani ni mshirika muhimu wa kibiashara kwa vile asilimia 8.7 ya bidhaa nje za Kenya ziliuzwa huko katika mwaka wa 2017 pekee, nyingi kati ya bidhaa nje hizi zikitokea kwenye viwanda vya kutengenezea nguo (WITS, n.d.).

Katika kipindi cha miongo miwili iliyopita, mapato ya Kenya kutokana na biashara nje nchini Marekani yaliongezeka kwa asilimia 285 (tazama Mchoro wa 6). Kuanzia 2014 hadi 2018, mapato ya Kenya ya kila mwaka kutokana na biashara nje nchini Marekani yalikuwa takriban Dola milioni 576 kwa kukadiria. Hasa, viwanda vya nguo vya Kenya ndivyo vilivyochangia pakubwa katika maendeleo haya, kwa vile vilichangia zaidi ya asilimia 60 ya bidhaa nje zote zilizouzwa nchini Marekani katika miaka ya hivi majuzi (tazama Kikasha cha 5). Kutokana na Serikali ya Marekani kupitisha sheria nzuri za biashara, kama vile Sheria ya mwaka wa 2000 ya Maendeleo na Fursa kwa Afrika (the 2000 African Growth and Opportunity Act) (AGOA), Marekani iliweza kuwa soko kubwa zaidi la ng’ambo la nguo ambazo zimetengenezwa nchini Kenya.

Kutokana na sheria hii ya AGOA, nchi za Afrika zinazostahili au kustahiki zinapendelewa, ikiwemo Kenya, jambo ambalo linawezesha karibu bidhaa zote zinazoweza kuuzwa sokoni kuingia kwenye soko la Marekani bila kutozwa kodi, zikiwemo nguo zilizotengenezwa viwandani, ambazo ndizo zimekuwa zikiuzwa sana baada ya sheria ya AGOA kuanza kutumika.

Sheria hii pia inaisadia serikali ya Kenya kufanikisha hatua za maendeleo katika nyanja zinazoleta maendeleo jumuishi na uongozi mzuri katika Ruwaza ya 2030—kukuza uchumi unaonawiri kutokana na masoko, kuimarisha utekelezaji wa sheria, kupambana na ufisadi, na kulinda haki za wafanyakazi—ambazo pia zinahitajika ili nchi iendelee kustahiki au kustahili kufaidika na AGOA (Mwakilishi wa Biashara wa Marekani).

Mchoro wa 6. Thamani ya mauzo ya nje ya Kenya kuelekea Marekani na mgawo wa nguo, 2000-2018

25 50 75 100% 200 400 600 $ milioni 800 2018 2015 2010 2005 2000 Thamani ya mauzo yote ya nje Asilimia ya mauzo ya nje ambayo yalikuwa nguo

Maelezo: Grafu hii inaonyesha jumla ya bidhaa zilizosafirishwa nje ya nchi na Kenya kwenda Marekani (nguzo za samawati) kati ya 2000 na 2018, na nguo kama asilimia ya jumla ya thamani ya bidhaa zilizosafirishwa nje ya nchi na Kenya kwenda Marekani (mstari wa samawati). Takwimu zote zimewekwa kwa msingi wa thamani isiyobadilika ya Dola ya 2019.

Asili: World Integrated Trade Solution (WITS), The World Bank.

Kikasha cha 5. Sheria ya Maendeleo na Fursa kwa Afrika (The African Growth and Opportunity Act) (AGOA) na kiwanda cha nguo cha Kenya

Sheria ya Maendeleo na Fursa kwa Afrika (The African Growth and Opportunity Act) ilipitishwa ili iwe sheria na Bunge la Marekani tarehe May 18, 2000. Sheria hii inaziwezesha nchi za kusini mwa Sahara za Afrika zinazostahiki zinazotimiza masharti mahususi ambayo yapo kwenye sheria hii kufikia soko la Marekani. Masharti haya yanahitaji nchi hizi husika zijitahidi kuimarisha utekelezaji wa sheria, haki za kibinadamu, na viwango au hali za kazi. Hapo awali, sheria hii ilipitishwa ili kutumika kwa kipindi cha miaka minane lakini baadaye kipindi hiki kiliendelezwa hadi mwaka wa 2025. Fungu maalum pia kuhusiana na nguo na mavazi yaliyotengenezwa viwandani liliongezwa kwa Sheria ya AGOA, ambalo lilihitaji nchi ya Marekani inunue nguo zilizotengenezwa viwandani kutoka katika nchi zinazostahiki kufaidika na AGOA kabla ya kununua kutoka nchi nyingine. Sharti hili la kupendelea nguo za nchi hizi zilizotengenezwa viwandani limechangia bidhaa nje za Kenya nchini Marekani ziongezeke.

Kilichogunduliwa 5: Wanafunzi, wasomi na wafanyakazi – stadi wa Kenya hunufaika kutokana na msaada wa kielimu na sera nzuri za uhamiaji za Marekani ili kuendeleza kazi zao.

Ni muhimu kuwekeza katika wafanyakazi wa Kenya ili wapate ujuzi mpya ambao ni muhimu katika jitahada za Kenya za kuwa na uchumi wa kisasa ambao unaendeshwa na sekta ndogo ya kilimo lakini yenye uzalishaji wa kiwango cha juu zaidi pamoja na ongezeko katika uzalishaji wa viwanda. Ili kusaidia utimizaji wa lengo hili, Serikali ya Marekani hufadhili fursa mbalimbali ili wanafunzi na wasomi wa Kenya waweze kuendeleza mafunzo na elimu yao katika taasisi za Marekani za elimu ya juu kupitia mipango yake ya viza iliyoundwa kwa ajili ya wanafunzi (viza za F-1) na wasomi (viza za J-1). Mchoro wa 7 unaonyesha idadi ya jumla ya wanafunzi na wasomi wapya wa Kenya wanaokwenda nchini Marekani kila mwaka kuanzia mwaka wa 2010 hadi 2018.

Mchoro wa 7. Idadi ya wanafunzi na wasomi wapya wa Kenya wanaokwenda nchini Marekani, 2010-2018

1,000 1,200 1,400 1,600 1,800 2,000 Number of people 18 15 2010

Maelezo: Grafu hii inaonyesha idadi ya wanafunzi na wasomi wapya wa Kenya waliopatiwa viza za kuenda Marekani kati ya mwaka wa 2010 na 2018.

Asili: U.S. Department of State.

Mbali na kuwapatia Wakenya fursa za kupata stadi mwafaka zinazohitajika ili kupata kazi zinazolipa vizuri, taasisi za Marekani pia hukuza viongozi, watalaam na watu wabunifu wa kizazi kijacho cha Kenya. Huku akiwa alihitimu kutoka Chuo cha Amherst katika jimbo la Massachusetts katika mwaka wa 1985 akiwa na shahada ya uchumi na elimu ya siasa, Rais Uhuru Kenyatta pengine ndio Mkenya anayetambulika zaidi leo hii ambaye alipokea elimu ya juu nchini Marekani.

Wanafunzi na wasomi wengi wa Kenya hupokea msaada wa kifedha katika kipindi cha kusoma kwao kupitia misaada ya kulipiwa masomo inayotolewa na mipango ya vyuo vikuu vya Marekani au mipango ya serikali ya Marekani, kama vile Mpango wa Fulbright Scholarship au Mpango wa Kimataifa wa Uongozi wa Wageni (the International Visitors Leadership Program) (IVLP). Tunakadiria kwamba wanafunzi na wasomi wa Kenya nchini Marekani hupokea angalau Dola milioni 19.6 kama msaada kila mwaka. Kiwango hiki tulichokadiria kinatokana na kiwango wastani cha wanafunzi 400 wa Kenya ambao walikuwa wakisomea shahada ya uzamivu katika Taasisi za Marekani katika mwaka wowote kati ya mwaka wa 2014 na 2019.[18]

Wanafunzi wakenya ambao wanasomea shahada za uzamivu nchini Marekani kwa kawaida hufadhiliwa kikamilifu na taasisi ambapo wanasomea, ikiwemo karo, bima ya afya na hela za kujikimu za kila mwezi.[19] Hii ni sehemu ndogo tu ya jumla ya msaada wa kielimu unaotolewa na Marekani kwa wanafunzi na wasomi wa Kenya, kwa vile wakenya wengine ambao wanasomea viwango vingine vya elimu (k.m, shahada ya kwanza, shahada ya uzamili, vyeti) pia wanaweza kupokea msaada wa kifedha kutoka kwa taasisi za elimu ambapo wanasomea.

Ingawa wanafunzi na wasomi wengi hurudi nchini Kenya baada ya kumaliza mipango yao ya elimu, baadhi yao huamua kujiunga na wafanyakazi wa Marekani ili kufanya kazi za kitaalam kupitia mpango wa viza ya H-1B. Mpango huu huwawezesha wafanyakazi wenye ustadi wa hali ya juu wanaotoka kwenye nchi za kigeni kujiunga na wafanyakazi wa Marekani na kupata ujuzi na uzoefu mwingine muhimu. Kuanzia mwaka wa 2014 hadi wa 2018, serikali ya Marekani ilipatiana viza 130 za H-1B kwa Wakenya kila mwaka. Huku kipindi cha viza kikiwa cha miaka 6 kwa wastani na mshahara wa kila mwaka ukiwa takriban Dola 80,600 kwa wapokeaji wa viza za H-1B, tunakadiria kihafidhina kwamba raia wa kenya walipata karibu Dola milioni 62.86 walipokuwa wameajiriwa nchini Marekeni.[20]

Kati ya mwaka wa 2009 na 2018, nchi ya Marekani ilipeana Ukaazi Halali wa Kudumu (LPR), almaarufu Green Card, kwa Wakenya 70,136. Watu ambao wana green card hii au hali hii halali wanastahiki kupata fursa mbalimbali za kazi ambazo hutamaniwa na watu wengi lakini haziwezi kupatikana na wahamiaji wengine. Kwa mujibu wa takwimu za Idara ya Kudumisha Usalama Ndani ya Nchi ya Marekani, Kenya iko kati ya nambari moja hadi tano miongoni mwa nchi za Afrika zenye idadi kubwa ya walio na Green Card. Wakenya wengi ambao ni LPRs na ambao ni wafanyakazi wa H-1B hudumisha uhusiano thabiti na Kenya na huendelea kusaidia familia, marafiki na jamii zao kwa kuwekeza kwenye biashara za Kenya na kwenye mali zisizohamishika, pamoja na kutuma pesa nchini Kenya.

Kilichogunduliwa 6: Dhamana za bima ambazo zimeungwa mkono na Serikali ya Marekani zimesaidia Kenya kuvutia takriban Dola milioni 742 ambazo zimewekezwa kwenye sekta ya kibinafsi tangu mwaka wa 2010.

Ruwaza ya 2030 ya Kenya inatambua umuhimu wa kuvutia Uwekezaji wa Kigeni wa Moja kwa Moja (FDI) ili kufadhili miundombinu ambayo nchi inahitaji kabisa. Dhamana za bima ambazo zimeungwa mkono na serikali ya Marekani huchangia pakubwa katika kuongeza imani ya wawekezaji wa kigeni watarajiwa kupitia kupunguza vikwazo vya kisiasa na kiuchumi vya kuwekeza katika uchumi wa Kenya.

Shirika la Marekani la Fedha na Maendeleo ya Kimataifa (The U.S. International Development Finance Corporation) (DFC), lililokuwa likijulikana hapo awali kama Shirika la Uwekezaji wa Kibinafsi Nje ya Nchi (Overseas Private Investment Corporation, OPIC), ni wakala huru ya serikali ambayo husaidia mashirika ya Kimarekani ambayo yanataka kufanya biashara na kuwekeza katika nchi zinazoendelea.[21] Kati ya mwaka wa 2010 na 2018, Serikali ya Marekani kupitia OPIC ilitoa msaada wa kifedha kati ya nchi mbili na bima ya hatari kwa ajili ya miradi 16 nchini Kenya, jumla ya fedha hizo ikiwa ni Dola milioni USD 664 (takriban Dola milioni 74 kila mwaka). Kiwango kikubwa cha fedha hizi kilichangia katika uwekezaji katika miradi ya miundombinu ili kuongeza viwango vya nishati inayoweza kutumiwa upya ambavyo Kenya inatoa (tazama Mchoro wa 8), ikiwa ni pamoja na Mradi wa Nishati ya Upepo wa Kipeto na upanuzi wa Stesheni ya Umeme wa Mvuke ya OrPower 4 (tazama Kikasha cha 6). Miradi mingine ilichangia katika maendeleo ya kiuchumi kwa kuimarisha ufikiaji wa huduma za benki, ujenzi wa shule na ujenzi wa nyumba, na vipengele muhimu vya kilimo.

Mchoro wa 8. Dhamana za uwekezaji za Marekani kwenye sekta ya nishati na sekta nyingine za Kenya, 2010-2018

MIGA, sekta nyingine MIGA, nishati inayoweza kutumiwa upya MIGA, nishati isiyoweza kutumiwa upya OPIC, sekta nyingine OPIC, nishati inayoweza kutumiwa upya $ milioni 597.1 67.4 40.8 36.4 0.3

Asili: DFC (formerly OPIC) and MIGA, the World Bank.

Vile vile, Marekani pia imeunga mkono shughuli za Wakala wa Kimataifa wa Udhamini wa Uwekezaji wa Benki ya Dunia (World Bank’s Multilateral Investment Guarantee Agency, MIGA) za kupatiana dhamana kwa mashirika yanayotaka kuwekeza nchini Kenya kutoka nchi zenye uchumi ulionawiri na zenye uchumi unaokua kwa kasi. Kupitia ufadhili wake muhimu kwa Jumuiya ya Maendeleo ya Kimataifa ya Benki ya Dunia, Marekani imefadhili takriban asilimia 12 ya dhamana za MIGA tangu 2010, ambayo ni Dola milioni 77 kati ya jumla ya Dola milioni 840.3 zilizotolewa kwa ajili ya miradi ya uwekezaji katika kipindi hicho (takriban Dola milioni 8.6 kwa mwaka). Fedha hizo zilifadhili miradi ya nishati inayoweza kutumika upya na isiyoweza kutumika upya pia, lakini nyingine zilifadhili huduma za benki, fedha na biashara za kilimo.

Kupitia dhamana zake za OPIC na MIGA, serikali ya Marekani imesaidia Kenya kuweza kuvutia Dola milioni 742 ambazo zimewekezwa kwenye sekta ya kibinafsi tangu 2010.

Kikasha cha 6. Mradi wa Nishati ya Upepo wa Kipeto na Stesheni ya Umeme wa Mvuke ya OrPower 4

Mradi wa Nishati ya Upepo wa Kipeto na upanuzi wa Stesheni ya Umeme wa Mvuke ya Olkaria III ndio miradi miwili kati ya mingine yenye thamani ya juu kabisa inayofadhiliwa na dhamana za uwekezaji za Marekani nchini Kenya, na yote miwili inadhihirisha kwamba watendaji/watoa msaada wa Marekani na njia nyingine za ufadhili za Marekani zimehusika. Kwa pamoja, miradi hii miwili inachangia pakubwa katika kufanikisha malengo ya Ruwaza ya 2030 ya Kenya ya kuimarisha ufikiaji wa umeme na utengenezaji wa vyanzo vipya vya nishati inayoweza kutumiwa upya (Ruwaza ya 2030).

Mradi wa Nishati ya Upepo wa Kipeto , ulioko kilomita 70 kusini magharibi mwa Nairobi, umekuwa ndio pahali ambapo uwanja mkubwa wa upepo umestahili kujengwa tangu serikali ya Ubelgiji iliposakinisha tabo za upepo hapo katika mwaka wa 1993 (Power Africa, 2019). Uwanja huo umeendelezwa sana hivi majuzi tu, kutokana na ushirikiano kati ya General Electric na (GE) Kipeto Energy Limited. Ushirikiano huu kati ya kampuni za Marekani na Kenya uliweza kuvutia ufadhili wa OPIC wa Dola milioni 232.56 katika mwaka wa 2015 (ambazo zilifika Dola milioni 251.16 katika mwaka wa 2019), takriban asilimia 72 ya gharama zote za mradi huo (DFC, 2020). Huku ikiwa pia na Dola milioni 50 ya ziada ya bima ya hatari iliyowekwa na OPIC katika mwaka wa 2018 (ambazo zilifika Dola milioni 51 katika mwaka wa 2019), uwanja huu wa upepo uliweka tabo ya kwanza ya upepo kati ya tabo 60 za GE zinazopaswa kuwekwa mnamo Desemba 2019 (Kipeto Energy, 2019). Ingawa ujenzi bado unaendelea, utakapokamilika, Uwanja wa Upepo wa Kipeto utazalisha megawati 100 za umeme, zitakazotosha kutoa umeme kwa nyumba 40,000 kwenye eneo hilo (General Electric, 2018).

Upanuzi wa stesheni ya umeme wa mvuke ya Olkaria III, iliyoko kilomita 90 kaskazini magharibi mwa Nairobi, pia unaonyesha njia nyingi ambazo Marekani inasaidia sekta ya nishati ya Kenya. Katika mwaka wa 2011, OPIC ilipeana dhamana ya uwekezaji ya Dola milioni 215.1 kwa Ormat Technologies (ambazo zilifika Dola milioni 245.3 katika mwaka wa 2019) ili kufadhili upanuzi, zikiambatana na dhamana ya uwekezaji ya MIGA ya Benki ya Dunia ya Dola milioni 134 (ambazo zilifika Dola milioni 152.8 katika mwaka wa 2019). Kutokana na msaada kutoka kwa dhamana hizi mbili za ziada za uwekezaji, stesheni ya umeme ya Olkaria III iliongeza kiwango cha nishati ambayo ilizalisha kutoka megawati 48 hadi megawati 84, kiwango ambacho karibu kiwe mara mbili ya kiwango chake cha kawaida cha uzalishaji (World Bank, 2020).

Kwenye sura hii, tumeangazia njia tatu ambazo serikali ya Marekani imetumia kuchangia maendeleo na ustawi wa Kenya. Hata hivyo, ushirikiano kati ya Marekani na Kenya umehusisha usaidizi kutoka kwa wengine ambao si serikali. Kwa kweli, Wahisani wa kibinafsi, kampuni, mashirika yasiyo ya kiserikali ya Marekani na watu binafsi wamekuza uhusiano wa karibu na washirika wao wa Kenya katika miongo miwili iliyopita. Kwenye sura inayofuata, tutazungumzia jinsi ambavyo mahusiano haya yanafaidi uchumi wa Kenya na watu wake.